Like Us On Facebook

MTOTO ANYOFOLEWA JICHO LAKE,MAMA MZAZI AWALILIA WATANZANIA WAMSAIDIE


MTOTO Khalidi Juma mwenye umri wa miaka minne, mkazi wa Vingunguti jijini Dar es Salaam, yuko katika mateso makali baada ya jicho lake moja kutolewa katika harakati za kumnusuru na ugonjwa wa Kansa, huku lingine nalo likilegea.

Akizungumza na mwandishi wetu, mama wa mtoto huyo Hadija Kilindo, alisema alimzaa mtoto huyo akiwa na afya njema, lakini alipofikisha umri wa miezi tisa ndipo alipogundua kitu cheupe kwenye mboni ya jicho lake.
 
Baada ya hali hiyo, alisema alimpeleka katika hospitali inayotibu watu wenye ulemavu mbalimbali ya CCBRT iliyopo Msasani jijini Dar, ambako baada ya kupimwa, aliambiwa mwanaye alikuwa na kansa.

“Baada ya kuambiwa mtoto wangu ana ugonjwa wa kansa sikuwa na jinsi, nilikubali afanyiwe upasuaji kwa ajili ya kuliondoa jicho hilo ili kuokoa maisha yake,” alisema.
 
Mama huyo alisema ilipofika mwaka 2012, jicho lingine lilianza kumuuma huku likiwa linavimba, lakini alipompeleka katika Hospitali ya Muhimbili, aliambiwa kansa imeshaenea mpaka kwenye ubungo, hivyo arudi naye nyumbani kwani hawezi kuishi kwa muda mrefu.
“Kwa kweli nilivyoambiwa hivyo nilinyong’onyea mwili mzima nikawa sina jinsi kabisa na nikapoteza matumaini kabisa ya mwanangu kuendelea kuishi tena,”alisema.
 
Alisema alirudi nyumbani huku maumivu ya kijana wake yakiendelea na mwishoni, jicho lake likawa halioni tena. Kuhusu jicho lililotolewa, mama huyo alisema alikuwa akilitoa na kulirudisha kwa ajili ya kulisafisha, lakini hivi sasa hawezi kulitoa tena kwa vile kuna nyama zilizolishika na hivyo kumsababishia maumivu makali mno mwanaye hasa kichwani.
 
“Unavyotuona hapa usiku hatulali kabisa, mtoto ni kulia kwa maumivu, amefikia wakati hawezi kula vizuri na anatumia muda mwingi kulia,” alisema.
 
Mama huyo aliongeza kueleza kuwa kutokana na hali ya mwanaye, anakosa muda wa kufanya chochote cha kujiingizi kipato, hivyo kuwa katika wakati mgumu mno kimaisha, hasa kwa vile baba mzazi wa mtoto huyo alimkimbia tokea alivyoanza kuumwa.

 
“Mimi naamini kabisa labda nikipata msaada nikienda hata kwa wachina nitapata hata dawa ya kumpunguzia mtoto wangu maumivu anayoyapata kwa hivi sasa,” alisema.
 
Kwa yeyote ambaye ataguswa na habari hii na angepeta kutoa msaada wa aina yo yote, anaweza kuwasiliana na mama mzazi anayetumia simu nambari 0656 042017.

-GPL
TOA MAONI YAKO KUHUSU HABARI HII
KAMA UMEGUSWA NA HABARI ZETU, TUNAOMBA UUNGANE NASI KATIKA PAGE YETU YA FACEBOOK HAPO CHINI. BOFYA "LIKE" KAMA BADO HUJA LIKE PAGE YETU.
 

KILELE CHA HABARI Copyright © 2014 -- Template created by Mbatta -- Powered by Kilelechahabari