Like Us On Facebook
Showing posts with label Katiba. Show all posts
Showing posts with label Katiba. Show all posts

HII NDO RASIMU YA PILI YA KATIBA MPYA ILIYOKABIDHIWA KWA RAIS KIKWETE LEO......JIPATIE NAKALA YAKO HAPA

 
Hii  ndo  Rasimu  ya  Pili  ya  Katiba  mpya  iliyokabidhiwa  kwa  Rais  Kikwete  leo...Nimejitahidi  kuikuza  ili  iweze  kusomeka  vizuri.... 

Rasimu  hii  ni  ndefu  kidogo, ina  ibara  271  ikilinganishwa  na  ile  ya  kwanza  ambayo  ilikuwa  na  ibara  240...

Rasimu  iko  hapo  chini, ukipabofya  itafunguka  kwenye  tab  mpya  ili  uweze  kuisoma  vizuri....Upande  wa  juu  kushoto  kuna  option  ya  kui download....

<< RASIMU YA  PILI, BOFYA  HAPA>>

Bofya  hapo  juu  uisome  rasimu  ya  pili  ya  katiba

DK. SENGODO MVUNGI AFARIKI DUNIA...!

Marehemu Dk. Sengondo Mvungi alipokuwa ICU katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Habari za kusikitisha zilizotufikia jioni hii zinasema kuwa Dk. Sengondo Mvungi amefariki dunia katika Hospitali ya Milpark Afrika Kusini alikokuwa akitibiwa. Dk. Mvungi alipelekwa wiki iliyopita Nov. 7 mwaka huu kwa ajili ya kupewa matibabu zaidi akitokea Hospitali ya Muhimbili kitengo cha MOI ambako muda wote alikuwa hajitambui baada ya kushambuliwa na majambazi na kuumizwa vibaya sehemu ya kichwani akiwa nyumbani kwake Kibamba. Wakati Dk. Mvungi anafariki, jana Jeshi la Polisi, kupitia  Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi, lilitangaza kuwakamata watuhumiwa 9 wakiwa na mapanga yaliyotumika katika uvamizi huo.
Mpaka mauti yanamfika, Dk. Mvungi alikuwa Mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba nchini na Mhadhiri Mwandamzi wa Sheria katika Chuo Kikuu cha Bagamayo (UB).
Marehemu aliwahi kugombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 kwa tiketi ya Chama cha NCCR-Mageuzi.

---CREDIT: GPL

VIDEO YA RAIS KIKWETE AKIONGEA NA VIONGOZI WA KAMBI YA UPINZANIA...NA HUU NDIO MUAFAKA ULIOFIKIWA JUU YA KATIBA MPYA

Rais Jakaya Kikwete na viongozi wa vyama vya siasa vya CCM, Chadema, CUF, NCCR- Mageuzi, TLP na UDP wamekubaliana mambo mawili makubwa baada ya kuweka pembeni tofauti za kiitikadi na kutanguliza masilahi ya taifa walipokutana jana Ikulu jijini Dar es Salaam.
Mkutano huo uliitishwa na Rais Kikwete ili kuondoa sintofahamu ya Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba uliopitishwa Septemba na Bunge lilipokutana mjini Dodoma.
Taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu jana jioni ilisema katika mkutano huo ilikubaliwa kwamba vyama vyote vya siasa nchini vyenye mawazo, maoni na mapendekezo ya kuboresha Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba viwasilishe mapendekezo yao haraka serikalini ili ifatutwe namna ya kuyashirikisha mapendekezo hayo katika marekebisho ya sheria hiyo.
Pia Rais na vyama hivyo walikubaliana kwamba vyama vya siasa nchini, kama wadau muhimu katika mchakato wa Katiba Mpya, viangalie namna ya kukutana na kujenga mfumo wa mawasiliano na maridhiano kwa lengo la kusukuma mbele mchakato huo kwa masilahi mapana ya nchi yao na mustakabali wa taifa.
“Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD) kimepewa jukumu la kuratibu jambo hilo ikiwa ni pamoja na kuandaa mkutano wa vyama hivyo na wadau wengine nchini,” iliongeza taarifa hiyo.
Viongozi wa vyama vyama vya siasa waliohudhuria mkutano huo ni Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia.
Wengine ni Makamu Mwenyekiti wa CCM, Philip Mangula, Isaack Cheyo ambaye alimwakilisha Mwenyekiti wa UDP, John Cheyo na Nancy Mrikaria ambaye alimwakilisha Mwenyekiti wa TLP, Augustine Mrema. Cheyo na Mrema wako nje ya nchi.
Wengine ambao waliambatana na wenyeviti wao ni Mohamed Mnyaa na Julius Mtatiro wa CUF, Tundu Lissu na John Mnyika wa Chadema na Martin Mng’ongo wa NCCR-Mageuzi.
Vicheko Ikulu
Vicheko na bashasha vyatawala Ikulu
Ilikuwa fursa kwa Rais Kikwete kukutana na viongozi hao baada ya kipindi cha miezi miwili cha kurushiana maneno baina ya viongozi wa Bunge, Serikali, CCM waliokuwa wakivutana na viongozi wa vyama vitatu vya Chadema, CUF na NCCR- Mageuzi.
Kama mtu yeyote angeulizwa kutabiri katika tukio lililotokea jana lingetokea basi angekuwa na wakati mgumu kutokana na ukali wa maneno na malumbano katika kipindi chote baada ya kumalizika kwa mkutano wa Bunge wa Septemba.
Rais Kikwete alionekana mwenye furaha tele wakati alipokutana na viongozi wa vyama hivyo na kivutio zaidi ilikuwa pale alipokutana na Mnadhimu Mkuu wa Kambi rasmi ya Upinzani, Tundu Lissu.
Viongozi hao walisalimiana huku wote wakitabasamu na kuashiria kuwa waliamua kuweka tofauti zao pembeni na kuangalia masilahi ya nchi.
Kumbuka katika hotuba yake ya mwisho wa mwezi Septemba, Rais Kikwete alimshutumu Lissu kwa kusema kwamba katika uteuzi wa wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba kuwa yeye hakuheshimu mawazo ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) na Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT).
Rais Kikwete alikaririwa akisema kauli hiyo ya Lissu ni uzushi, uongo na uzandiki wa hali ya juu, huku akisisitiza kuwa mbunge huyo alitoa kauli hiyo ili kupotosha ukweli na pengine isaidie kujenga hoja yake ya kutaka Rais asiteue wajumbe 166 wa Bunge Maalum la Katiba.
Lissu, ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki, alipinga tuhuma hizo na kusisitiza Rais aliteua wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba kutoka Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC) na Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT) bila ya ridhaa yao.
Chikawe, Wassira na Lukuvi ndani
Mawaziri watatu, ambao walitetea kwa nguvu kupitishwa kwa muswada ule ndani na nje ya Bunge walihudhuria mazungumzo hayo.
Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Uratibu na Bunge, William Lukuvi, Waziri wa Sheria na Katiba, Mathias Chikawe na Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Rais anayeshughulikia Mahusiano na Uratibu, Stephen Wassira walikuwemo kwenye mazungumzo ya jana.
Mawaziri hawa kwa nyakati tofauti walitetea kuwa mchakato wa muswada ule haukuwa na matatizo yeyote na kushikilia kuwa lazima Rais lazima asaini muswada kwani ulikuwa umepitishwa kihalali na Bunge.
Pia walikuwa wameshikilia kuwa safari hii kulikuwa hakuna mambo ya mazungumzo kati ya Rais na upinzani.

Chanzo cha sintofahamu
Wabunge wa vyama vya Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi walisusia mjadala wa muswada huo wakipinga matayarisho yake kutoshirikisha upande wa Zanzibar na pia walikuwa hawakubaliani na baadhi ya vipengele vya muswada huo.
Katika hatua nyingine, taarifa kutoka Ikulu zilisema kwamba Rais Kikwete alisaini muswada huo tangu Oktoba 10 mwaka huu siku ambayo wapinzani walipanga kufanya maandamano nchi nzima.
Katika mahojiano na Mwananchi jana jioni, Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Salva Rweyemamu alisema muswada huo tayari ulikwishasainiwa na Rais na kama kuna marekebisho yatafanywa.
Mwananchi ilimtafuta Rweyemamu baada ya kusikia akithibitisha kusainiwa kwa muswada huo katika mahojiano na BBC Idhaa ya Kiswahili jana.
Akizungumza na Mwananchi Rweyemamu alisema, “Rais ameshasaini tangu Oktoba 10, unajua kulikuwa hakuna tatizo lolote kuhusu muswada huu kwa sababu ulifuata taratibu zote bungeni.”
Rweyemamu alisema kuwa awali Ikulu ilitoa taarifa kuwa Rais atakutana na wapinzani, pia atausaini muswada huo.
“Muswada umepitishwa bungeni na yeye amekamilisha kazi kwa kuusaini ili kuwa sheria. Alipokutana na wapinzani leo (jana) amewaeleza hilo na wameridhika” alisema Rweyemamu.
 CHEKI VIDEO HAPO CHINI....

"KATIBA MPYA ITAMKE KUOLEWA KUANZIA MIAKA 18"....CHIKAWE

            Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe, amesema anatarajia Katiba Mpya itabainisha umri wa msichana kuolewa ni miaka 18 na kuondoa utata wa kisheria na kukomesha ndoa za utotoni.
Aliyasema hayo jana jijini Dar es Salaam katika kikao cha wadau mbalimbali kujadili namna ya kukomesha ndoa za utotoni ikiwa sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Mtoto wa Kike Duniani.
Waziri Chikawe alisema kwa sasa kuna mkanganyiko wa Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 inayobainisha kuwa mwanamke na mwanaume wawe wametimiza umri wa miaka 18 ili wafunge ndoa, hata hivyo mwanamke anaweza kuolewa akiwa na umri wa chini ya miaka18 lakini siyo chini ya miaka 15 kama atapata idhini ya wazazi au kama wote wamefariki idhini itatolewa na mlezi wa binti huyo.
“Kisheria mtoto mwenye umri chini ya miaka 18 hawezi kuingia kwenye mkataba. Na Sheria ya Makosa ya Kujamiiana ya mwaka 1998 (SOSPA) inatamka wazi kuwa mwanamume atajayejamiiana na msichana mwenye umri chini ya miaka 18 hata kama ameridhia ni mbakaji na atahukumiwa kwa mujibu wa sheria.Huu ni mgongano wa kisheria,”alisema.
Alisema hatua hiyo itasaidia kujenga mazingira mazuri ya kukomesha ndoa za utotoni na kuwapa fursa wasichana kukua vyema na kupata elimu ambayo ni haki yao ya msingi.
Mkurugenzi wa Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (Tamwa),Valerie Msoka alisema anatiwa moyo na hatua hiyo ya serikali, lakini akatoa angalizo kwamba kuwa na sheria nzuri ni jambo na utekelezaji ni jambo jingine “tunataka kuona utekelezaji wa vitendo ili kuwanusuru wasichana na ndoa za utotoni,” alisema.
Mke wa Rais wa Afrika Kusini, Graca Machel, katika ujumbe wake kwa nijia ya video alisema ni muhimu kukaimarisha usajili wa ndoa na vifo vya wasichana wadogo ili ukubwa wa tatizo lifahamike na kuhakikisha kuwa watoto wanapata fursa ya elimu, kuondoa umaskini na haja ya kukomesha ndoa za utotoni.
Tanzania ni miongoni mwa nchi zenye kiwang cha juu cha ndoa za utotoni duniani na inakadiriwa kuwa wasichana wawili wa Tanzania kati ya watano watakuwa wameolewa kabla ya kufikisha umri wa miaka 18.Kiwango hiki cha juu kinachangia kukwamisha wasichana kupata elimu, kupata mimba na kuhatarisha maisha yao kutokana na matatizo ya afya ya uzazi.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI   

KATIBA YAMVURUGA RAIS KIKWETE....WAPINZANI WAMPA MASHARTI MAZITO KUKUTANA NAE KABLA YA TAREHE 10....

                    SIKU moja baada ya Rais Jakaya Kikwete kuvisihi vyama vya CHADEMA, CUF na NCCR-Mageuzi kusitisha maandamano yao na kurejea meza ya mazungumzo ili kupata muafaka wa muswada wa sheria ya kubadili sheria ya mabadiliko ya katiba, vyama hivyo vimetoa masharti mazito ya kukutana naye.

Hatua hiyo inakuja wakati vyama hivyo vikiendelea kushikilia msimamo wao wa kuitisha maandamano ya nchi nzima kupinga muswada huo, wanaodai kuwa unalenga kuipa CCM nafasi ya kuhodhi mchakato wa katiba mpya.

Wakati vyama hivyo vikiwa vimefanya mikutano ya ndani na makundi mbalimbali, na kisha mikutano miwili ya hadhara Dar es Salaam na Zanzibar, CCM nayo inakazana kumshinikiza rais asaini muswada huo kama ulivyopitishwa na Bunge.

Tanzania Daima Jumapili limedokezwa kuwepo mvutano mkali ndani ya CCM, ambako makundi ya vigogo wanaotajwa kugombea urais mwaka 2015, wanampinga Rais Kikwete kwa jinsi anavyoendesha mchakato huo, wakidai anawabeba wapinzani.
  
Licha ya wadadisi wa masuala ya kisiasa kumtabiria Rais Kikwete kuwa anaweza kujiandikia historia nzuri endapo mchakato huo ukifanikiwa kwa kuzingatia matakwa ya wananchi, CCM inamtazama mwenyekiti huyo kama anataka kuwakomoa wenzake.
  
“Kuna msuguano mkali ndani ya CCM, Rais Kikwete ana nia njema na mchakato huu ili ukamilike kwa amani, lakini wenzake ndani ya chama wanadhani anataka kuwanufaisha wapinzani kwani hatakuwa na chochote cha kupoteza,” alisema kigogo mmoja wa CCM.
  
Ni katika nia njema hiyo Rais Kikwete katika hotuba yake ya mwisho wa mwezi, aliwasihi viongozi wa vyama vitatu vya upinzani kutoandamana, badala yake wakae na kutafuta njia mbadala ya kisheria kuboresha muswada huo, na kwamba serikali iko tayari kuwasikiliza.
  
Hata hivyo, wito wa Rais Kikwete umepokelewa kwa taswira tofauti na vyama hivyo, vikisema kuwa yeye ndiye anapaswa kuwaandikia barua kuwaomba akutane nao kwa mazungumzo Ikulu, kwani wao hawajawahi kuomba kukutana naye.

Badala yake, vyama hivyo vilisisitiza kuwa viliomba kukutana na wadau mbalimbali na wananchi kumshinikiza asisaini muswada, na kwamba msimamo wao uko pale pale.

Katika msimamo huo, vyama hivyo vimesema maandamano yaliyotangazwa kufanyika Oktoba 10 nchi nzima yako pale pale, na kamati ya maandalizi inaendelea kufanya taratibu zote.
  
Wakizungumza jana jijini Dar es Salaam, wawakilishi wa vyama hivyo, John Mnyika (CHADEMA), Faustine Sungura (NCCR-Mageuzi) na Abdul Kambaya (CUF), walisema kuwa kamati ya maandalizi ya maandamano inaendelea kwa kuwa Rais Kikwete katika hotuba yake hakugusia suala lolote kama atasaini muswada huo au la.
  
“Rais amezungumzia hoja za upinzani za kuvunjwa kwa Tume ya Jaji Joseph Warioba kabla ya kumaliza muda wake, kwa hili tunampongeza, amekuwa wazi. Lakini afahamu kuwa hiyo si hoja kuu iliyosababisha tuandae maandamano kushinikiza asisaini huo muswada.
  
“Mambo mengine mazito yapo, kuhusu muundo wa Bunge la Katiba na idadi ya wajumbe kwa uwiano sawa wa Zanzibar na Tanganyika na kuhusu maoni ya wadau kuachwa,” alisema Mnyika.

Alisema kuwa maoni ya wadau yamepuuzwa, uchakachuaji umefanyika, taasisi zilipeleka majina, lakini Rais Kikwete anasema kuwa alizingatia hilo, kwamba wanamwomba aseme kwanini hakuchukua jina kati ya yale yaliyopendekezwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Shirikisho la Vyama vya Wenye Ulemavu (Shiwavyata) na CCT.
  
Alisema kuwa hao walijitokeza kwenye kamati wala hawakusema kwa siri, hivyo Rais Kikwete awaambie mawaziri wake wamwambie ukweli.

Alihoji kuwa Rais Kikwete katika hotuba yake ametumia neno ‘nimeambiwa’ kwa kiasi kikubwa, kwamba ingefaa mawaziri wake hasa Waziri wa Sera, Uratibu na Bunge, William Lukuvi; Waziri wa Sheria na Katiba, Mathias Chikawe; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mahusiano na Uratibu, Stephen Wassira na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba wamwambie ukweli.
  
“Huyu huyu rais ndie aliwaambia wafanyakazi wakati wa mgomo wao kuwa akili za kuambiwa na viongozi wao wachanganye na za kwao, kwanini katika mambo aliyoambiwa na wasaidizi wake hakujiridhisha kwanza?” alihoji.
  
Hivi karibuni, Waziri Wassira aliwakejeli wapinzani kuwa wasitarajie tena kukaribishwa Ikulu, kutokana na msimamo wao wa kususia mjadala wa muswada wa marekebisho ya sheria ya mabadiliko ya katiba wa mwaka 2013.
  
Alisema kuwa maandamano yaliyokuwa yanaandaliwa kumshinikiza rais asisaini muswada huo, hayana maana kwani rais hana sababu za kutousaini.
  
Licha ya Wassira kudai milango ya wapinzani kuzungumza na rais katika suala hilo imefungwa, Rais Kikwete amewasihi wapinzani wakae na serikali wajadili kasoro zilizopo kwenye muswada kama walivyofanya mwaka 2011 wakati mchakato unaanza hatua ya kwanza.
  
Hata Waziri Chikawe naye alimtisha rais hivi karibuni kuwa iwapo ataliafiki suala hilo la wapinzani na makundi mengine, na kuacha kutia saini muswada huo, atakuwa ametengeneza mgogoro na mhimili wa Bunge kutokana na chombo hicho kukamilisha kazi yake.
  
Lakini rais amewapuuza mawaziri wake hao na kutumia busara akisema kuhusu hoja ya Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria kutokufanya vikao Zanzibar kusikiliza maoni ya wadau, saula hilo lilianzia bungeni hivyo linaweza kurudishwa huko lijadiliwe tena.

Kuhusu rais kumwandama Msemaji wa Kambi ya Upinzani, Tundu Lissu kuwa alisema uongo bungeni, Mnyika alisema hakufanya vema kumshambulia mbunge huyo kwani hayo hayakuwa mawazo yake binafsi bali maoni ya kambi ya upinzani.
  
“Inakuwa sio vizuri mbunge aliyetoa mawazo bungeni kwa mujibu wa katiba na kanuni za Bunge kushambuliwa kwa maneno makali na rais wakati alikuwa anatoa mawazo ya kambi wala si yake,” alisema Mnyika.

Lissu ajibu
Akizungumza na gazeti hili, Lissu amehoji hotuba ya Rais Kikwete iliyojaa neno “nimeambiwa” akisema ana uhakika gani wale waliomwambia kama hawakumdanganya?

“Maneno yaliyotajwa na rais kuhusu uteuzi wa wajumbe toka Shirikisho la Vyama vya Wenye Ulemavu, TEC na CCT yalizungumzwa kwenye kamati sio maneno yangu. Kikwete hakuwepo kwenye kamati, mimi nilikuwepo. Sasa mawaziri wake na wabunge wake wa CCM wamwambie ukweli, waache kumdanganya.

“Kikwete amesema mimi ni muongo, mnafiki, lakini hoja ambazo tulizipinga mfano ya ushiriki wa wadau wa Zanzibar, hata Waziri wa Sheria na Katiba wa Zanzibar, Abubakari Khamisi naye ameniunga mkono. Je, na huyu ni mzushi, muongo na mfitini?” alihoji.

Aliongeza kuwa hoja ambayo rais anakimbilia kwamba alimzuia asiteue wajumbe 166, ilikuja bungeni mwaka 2011, wakaipinga, ikaondolewa. Lakini mwaka huu wameirejesha tena.

WARIOBA AWATAKA WANASIASA WAACHE KUIJADILI TUME YAKE NA BADALA YAKE WAJADILI RASIMU YA KATIBA KWA MANUFAA YA WATANZANIA


              MWENYEKITI wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba, amewataka wanasiasa kujielekeza katika kuijadili rasimu ya Katiba iliyotolewa badala ya kuijadili tume na wajumbe wake.
 
Jaji Warioba alisema tume yake siku zote imekubali kukosolewa kwa kuamini kuwa ni jambo la kawaida lakini akaongeza kwamba ni vema wananchi na wanasiasa wakajadili rasimu ya Katiba iliyotolewa.
 
“Nadhani wangezungumzia rasimu wangetusaidia sana, badala ya kuzungumzia tume na watu.
 
“Na siamini kama kauli za viongozi hao wa kisiasa ndiyo misimamo ya vyama vyao,” alisema.
 
Jaji Warioba alitoa kauli hiyo jana wakati akikanusha tuhuma zilizoelekezwa kwa tume yake na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Abdallah Bulembo, kwamba tume hiyo imeacha kutekeleza majukumu yake na kuingilia uhuru wa wananchi wa kutoa maoni.

Alisema kuwa siku zote tume yake imekuwa ikitekeleza majukumu yake kwa kuzingatia sheria na kuwataka wanasiasa hao kujadili rasimu iliyotolewa badala ya kuishambulia tume au wajumbe wake.
 
“Moja ya kazi za kisheria za tume ni kutoa elimu kwa umma, na ni kazi ya wakati wote,” alisema.
 
Bulembo alinukuliwa na baadhi ya vyombo vya habari juzi akiwa mkoani Tanga ambapo alisema kuwa Tume ya Warioba imeacha kutekeleza majukumu yake na kuingilia uhuru wa wananchi wa kutoa maoni.

Akijibu upotoshaji huo, Jaji Warioba alisema kuwa katika mikutano ya mabaraza ya Katiba ya Wilaya, wananchi ambao walikuwa ni wajumbe wa mabaraza hayo walikuwa na fursa ya kuuliza maswali na wajumbe wa tume walitoa elimu kuhusu hoja na maswali yaliyoulizwa kwa mujibu wa sheria.
 
“Sasa Bulembo anaona kutoa elimu ni dhambi?” aliuliza Warioba ambaye amewahi kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais.
 
Jaji Warioba alikumbusha kuwa tume yake imekuwa ikifanya kazi katika mazingira magumu kutokana na kauli za wanasiasa mbalimbali na kuongeza kuwa pamoja na kauli hizo tume yake inafarijika na kauli za kutia moyo wanazozipata kutoka kwa wananchi wa kawaida.
 
“Nilisema mwishoni mwa mwezi uliopita wanasiasa wamekuwa wakitoa matamshi yaliyoifanya kazi ya tume kuwa ngumu katika mikutano ya mabaraza ya Katiba.

“Matamshi mengine yalilenga tume na wakati mwingine yalinilenga mimi binafsi au wajumbe wa tume badala ya kuzungumzia rasimu,” alisema.

-Tanzania daima

MAELFU YA WANANCHI WAJITOKEZA KATIKA MKUTANO WA CHADEMA,NCCR, CUF HUKO JANGWANI JIJINI DAR.


     Maelfu  wakazi wa jiji la Dar es salaam  wengi wao wakiwa ni  wafuasi wa vyama vya Chadema ,Cuf na NCCR Mageuzi  wemefurika katika  viwanja vya jangwani kuwasilikza  viongozi wakuu wa vyama hivyo ambapo kwa pamoja viongozi hao  wanapinga  hatua  ya serikali  kuingiza baadhi ya vipengele  katika mswada wa  sheria  ya marekebisho  ya  sheria  ya mabadiliko ya katiba .

Viongozi  hao  wanadai  kuwa  vipengele hivyo vitapelekea kupatikana kwa katiba  ya upande mmoja  na kuongeza kuwa kama mswada huo hautafanyiwa marekebisho, basi  wao  hawatashiriki katika bunge la katiba.
  
Katika viwanja hivyo  ulinzi uliimarishwa kutoka katika vikundi mbalimbali  vinavyomilikiwa na vyama hivyo  huku shamra shamra za huko na kule zikiwa hazikosekani ili mradi kunogesha mkutano.
 

Mwenyekiti wa taifa wa Chadema  na ambaye  ni kiongozi wa kambi ya upinzani bungeni Mh Freeman Mbowe amewataka watanzania kuacha uoga na wasimame imara kudai katiba bora.
 

Naye mwenyekiti wa Cuf Mh Profesa Ibrahim Lipumba  amesema Tanzani inahitaji katiba ambayo italinda na kusimamia rasilimali za taifa  kuweza kutimia kwa usawa na kuzingatia mahitaji ya watanzania wenyewe.
 
Kwa upande wake mwenyekiti wa NCCR Mageuzi  na mbuge wa kuteuliwa amesema hakuna haja ya kutumia  mabavu  na badala yake ameitaka serikali itumie busara zaidi ili kuweza kufikia  mwafaka wa jambo hili.

CHIKAWE:HAKUNA SHERIA INAYOMBANA KIKWETE ASISAINI MSWADA WA SHERIA,MAANDAMANO YA WAPINZANI HAYATASAIDIA KITU



Waziri wa Katiba na Sheria, Mathis Chikawe amesema Rais Jakaya Kikwete hana mpango wa kuongeza muda wa uongozi wake baada ya 2015 kama baadhi ya wanasiasa wanavyodai. 

Kadhalika, waziri huyo amesema hakuna sheria inayomlazimisha Rais kusaini muswada wa sheria yoyote inayopitishwa na Bunge na wala inayoweka muda maalumu wa kutekeleza wajibu huo.
 

Akizungumza na gazeti hili jana, Chikawe alisema kwa vyovyote vile Rais Kikwete hawezi kuongeza muda wa kuwapo kwake madarakani kwa kuwa anaheshimu Katiba ya nchi iliyomuweka madarakani.
 

Waziri huyo alitoa kauli hiyo baada ya kutakiwa na gazeti hili kuzungumzia madai ambayo yamekuwa yakirudiwa mara kwa mara na Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba kwamba amenasa taarifa za siri za kuwapo kwa mipango ya kuongeza muda wa Serikali ya sasa kukaa madarakani.
 

“Ngoja nikwambie ndugu yangu, watu wanaongea tu, kwanza Rais mwenyewe hana mpango huo, anasema kazi aliyonayo ni ngumu na haoni sababu ya kuongeza muda,”alisema Chikawe na kuongeza:
 

“Mara zote ukizungumza naye anasema tuharakishe mchakato wa Katiba na ikibidi tuingie katika Uchaguzi Mkuu wa 2015 kama Katiba yetu inavyosema kwa kuwa kazi aliyofanya inatosha kabisa.”
 

Mapema mwezi Mei mwaka huu, Profesa Lipumba alisema kutokana na wasiwasi kwamba mchakato wa Katiba Mpya hautakamilika 2014, hivyo Uchaguzi Mkuu hautaweza kufanyika.
 

Kuhusu hatima ya Uchaguzi Mkuu iwapo Katiba Mpya itaanzisha mfumo wa Serikali tatu, Chikawe alisema: “Wananchi wasiwe na wasiwasi ikifika wakati huo kila kitu tutajua, lazima tutakuwa na sheria ya mpito ambayo itaweka mambo sawa mpaka kutufikisha katika Uchaguzi Mkuu.”


Rais kusaini muswada

Chikawe pia alizungumzia hatima ya Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba Mpya ambapo alisema hakuna sheria inayomlazimisha Rais kusaini miswada inayopitishwa na Bunge.

“Hakuna sheria inayomlazimisha Rais asaini wala kumpa muda wa kusaini, mwenyewe anatumia busara na hekima tu katika kusaini sheria,”alisisitiza Chikawe.
 

Kauli ya Chikawe imekuja siku chache baada ya wenyeviti wa vyama vya CUF, NCCR -Mageuzi na Chadema kutoa tamko la kumtaka Rais Kikwete asisaini muswada huo mpaka pale yatakapokuwapo maridhiano ya wadau muhimu kuhusu muswada huo. 

Alisema kwa kutokusaini muswada huo, kunaweza kukaleta tafsiri mbili; kwanza ni wale wanaoweza kutafsiri kuwa ni dharau kwa wabunge waliopitisha muswada huo, kwamba walichofanya si sahihi na hakina maana.


Hoja ya pili alisema kwa kutosaini pia kunaweza kuzidisha msukumo kwa wanachama wa chama chake, lakini pia kutoka kwa wananchi ambao wanasubiri kwa hamu utekelezaji wa sheria hiyo.
 
Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba wa 2013 ambao ulipitishwa na mkutano wa Bunge uliopita baada ya mvutano mkali, umeendelea nje ya Bunge, huku kukiwa na madai kwamba ulipitishwa ukiwa na marekebisho ambayo yalifanyika kinyume na maoni ya wadau.
 
Madai mengine ni kwamba wabunge wa CCM waliongeza baadhi ya mambo kupitia majedwali ya marekebisho, hivyo kutoa mwanya kwa Serikali inayoongozwa na chama hicho kupitia kwa Rais kuwa na mamlaka zaidi ya uteuzi wa wajumbe husika.
 
Septemba 6 mwaka huu, wabunge wa CCM walitumia wingi wao kupitisha muswada huo katika mkutano wa Bunge ambao ulisababisha tafrani kiasi cha Mbowe na Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi kutolewa nje ya Bunge kwa amri ya Naibu Spika, Job Ndugai.
 
Katika tafrani hiyo, baadhi ya wabunge wa upinzani walirushiana makonde na askari wa Bunge, huku wabunge wote wa upinzani, isipokuwa Mbunge wa Vunjo (TLP), Augustine Mrema, wakisusia vikao vya muswada huo.

-Mwananchi
 

KILELE CHA HABARI Copyright © 2014 -- Template created by Mbatta -- Powered by Kilelechahabari