Like Us On Facebook

AKINA SAMATTA, ULIMWENGU WAANZIA UGENINI NUSU FAINALI AFRIKA NA MAZEMBE YAO

             TOUT Puissant Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), itaanzia ugenini Nusu Fainali ya kwanza ya Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Stade Malien ya Mali, Oktoba 6, mwaka huu, kabla ya kurudiana wiki mbili baadaye mjini Lubumbashi.Kwa mujibu wa Ratiba iliyotolewa na Shirikisho la Soka Afrika (CAF) jana, mchezo wa kwanza utachezwa kwenye Uwanja wa Modibo Keita mjini Bamako kuanzia saa 10:00 jioni kwa saa za huko na saa 12:00 kwa saa za Afrika Mashariki.
Mapacha watatu; Kutoka kulia Thomas Ulimwengu, Tresor Mputu na Mbwana Samatta washambuliaji hatari wa Mazembe ambao wanafunga karibu kila mechi
Mechi hiyo itachezeshwa na refa Alioum Neant, atakayesaidiwa na Evarist Menkouande wote wa Cameroon na Peter Edibi wa Nigeria, wakati refa wa akiba atakuwa Mohamadou Mal Souley pia wa Cameroon.Timu hizo zitarudiana Oktoba 19, Uwanja wa Mazembe mjini Lubumbashi, zikichezeshwa na marefa Haimoudi Djamel wa Algeria atakayesaidiwa na Achik Redouane wa Morocco na Etchiali Abdelhak wa Algeria, wakati refa wa akiba atakuwa Bousseter Sofiane  wa Algeria pia.Mazembe inayoongozwa na washambuliaji wawili wa Kitanzania, Mbwana Ally Samatta na Thomas Emmanuel Ulimwengu, ikifanikiwa kuitoa Stade Malien itamenyana na mshindi wa Nusu nyingine, kati ya timu za Tunisia tupu, Club Africaine na C.S. Sfaxien.Ikumbukwe Mazembe iliangukia kwenye Kombe la Shirikisho baada ya kutolewa na Orlando Pirates ya Afrika Kusini katika 16 Bora ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu huu na sasa inaelekea kufuta machungu kwa kutwaa taji hilo la pili kwa ukubwa kwa michuano ya klabu Afrika.
TOA MAONI YAKO KUHUSU HABARI HII
KAMA UMEGUSWA NA HABARI ZETU, TUNAOMBA UUNGANE NASI KATIKA PAGE YETU YA FACEBOOK HAPO CHINI. BOFYA "LIKE" KAMA BADO HUJA LIKE PAGE YETU.
 

KILELE CHA HABARI Copyright © 2014 -- Template created by Mbatta -- Powered by Kilelechahabari