Like Us On Facebook

WATU 9 WATIWA MBARONI KWA TUHUMA ZA KUMCHARANGA MAPANGA DR SENGONDO MVUNGI


WATU tisa wanashikiliwa na Polisi Dar es Salaam kwa tuhuma za kuvamia nyumbani na kumjeruhi Mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba na mwanasheria mkongwe, Dk Sengondo Mvungi.
 
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emannuel Nchimbi alisema jana Dar es Salaam kuwa baadhi ya watuhumiwa hao walikutwa na simu iliyoporwa nyumbani kwa Dk Mvungi pamoja na mapanga yanayodaiwa kutumika katika shambulizi hilo.
 
Dk Mvungi alivamiwa na kushambuliwa wiki iliyopita nyumbani kwake Kibamba na kupoteza fahamu kukimbizwa katika Hospitali ya Tumbi, Kibaha kabla ya kuhamishiwa Muhimbili ambako alilazwa katika Taasisi ya Mifupa (MOI) na kishsa kupelekwa Milpark, Afrika Kusini ambako anatibiwa.
 
Waziri Nchimbi alisema baada ya mahojiano ya kina washukiwa hao walikiri kushiriki tukio hilo na walitoa ushirikiano wa kutosha hadi kupatikana kwa mapanga hayo na kigoda.
 
“Uchunguzi wa Polisi katika tukio hili umekamilika kwa asilimia 80, tumebakiza watu wachache walioshiriki na tunawahakikishia wananchi kuwa tutawakamata hivi karibuni,” alisema Nchimbi ambaye alifuatana na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Pereira Ame Silima na Mkuu wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova.
 
Kova alitaja waliokamatwa kuwa ni Msigwa Mpopera ambaye ni mlinzi nyumbani kwa Dk Mvungi ambaye kwa mujibu wa Kova ndiye alikuwa kiongozi wa tukio hilo na kwamba aliongoza wenzake kufanya shambulio hilo.
 
Mwingine ni Chibango Magozi ambaye alikamatwa akiwa na simu iliyoibwa nyumbani kwa Dk Mvungi. Kamanda Kova alisema baada ya watuhumiwa hao kubanwa walitaja wenzao na kukubali kwenda kuonesha mapanga waliyotumia kutenda uhalifu huo.
 
Wengine wanaoshikiliwa ni Ahmed Ali, Zakaria Msesa, Manda Saluwa, Paul Jailos na Juma Khamis ambao wote ni wakazi wa Vingunguti; Longishu Semariki mwuza tumbaku (ugoro) katika eneo la Msimbazi na Msunga Makenza dereva wa bodaboda Kitunda.
 
“Upelelezi wa tukio hili umefanywa kwa kiwango cha juu na tunashukuru ushirikiano uliooneshwa na familia na vyombo vya habari,” alisema Kamanda Kova.
 
Alisema kazi iliyobaki sasa ni kukamilisha upelelezi na kupeleka jalada kwa Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) ili atoe kibali cha kesi hiyo kwenda mahakamani.
 
Akijibu maswali ya waandishi wa habari, Kova alisema uhalifu aliofanyiwa Dk Mvungi hauhusiani na siasa kwani ushahidi unaonesha kuwa watuhumiwa walikuwa wanatafuta kipato.
 
Ulimboka, Kibanda
Alipoulizwa sababu ya upelelezi wa tukio la Dk Mvungi kuharakishwa, wakati kuna matukio kama ya Mhariri Mtendaji wa New Habari, Absalom Kibanda na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari, Dk Steven Ulimboka hadi leo Polisi iko kimya, Kova alisema watuhumiwa wa Dk Mvungi walipatikana haraka kutokana na ushirikiano wa vyombo vya habari na familia.
 
“Unajua katika tukio hili hazikuwapo habari za Polisi kuhusika au mhusika ni nani, haya mambo ya upelelezi ukishamtuhumu polisi wakati ndiye anafanya upelelezi wakati mwingine inakatisha tamaa,” alisema Kova.
 
Dk Nchimbi alifafanua kuwa matukio ya Dk Ulimboka na Kibanda yanaendelea kufanyiwa uchunguzi.
 
“Katika nchi zinazoendelea, upelelezi wa matukio mengine unafanyika hata miaka mitatu au minne na baadaye watuhumiwa wanakamatwa kirahisi.”
 
Wakati huo huo, Dk Nchimbi alisema katika kupambana na uhalifu nchini, Polisi itasambaza maofisa wake wapatao 200 kila tarafa ambao watashirikiana na Polisi Jamii kupambana na uhalifu.
-Habari leo
TOA MAONI YAKO KUHUSU HABARI HII
KAMA UMEGUSWA NA HABARI ZETU, TUNAOMBA UUNGANE NASI KATIKA PAGE YETU YA FACEBOOK HAPO CHINI. BOFYA "LIKE" KAMA BADO HUJA LIKE PAGE YETU.
 

KILELE CHA HABARI Copyright © 2014 -- Template created by Mbatta -- Powered by Kilelechahabari