Like Us On Facebook

Watanzania wanne wafikishwa mahakamani kwa kosa la kujiunga na kundi la Al Shabaab


WATU wanne wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, wakikabiliwa na mashitaka ya kuwa wanachama wa kundi la kigaidi la Al Shabaab. Washitakiwa hao waliofikishwa mahakamani jana ni Ally Rashid, Shaban Waziri, Faraji Ramadhani na Mussa Mtweve.
Wakili wa Serikali, Peter Maugo alidai mbele ya Hakimu Mkazi Sundi Fimbo, kuwa kati ya Januari 11 mwaka jana na Septemba 16 mwaka huu, eneo la Kibaoni, Dar es Salaam, Rashid alisajili washitakiwa wenzake kuwa wanachama wa kundi hilo.
 
Aliendelea kudai, kuwa katika siku hizo, washitakiwa walikamatwa kwa kuwa wanachama wa kundi la kigaidi la Al Shabaab ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambalo pia linafanya shughuli zake Kenya na Somalia.
 
Washitakiwa hao hawakutakiwa kujibu mashitaka kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo isipokuwa Mahakama Kuu ya Tanzania.
 
Aidha, upande wa mashitaka ulidai kuwa upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika na washitakiwa walirudishwa rumande hadi Desemba 5 kesi hiyo itakapotajwa.
 
Kesi hiyo imefunguliwa katika Mahakama ya Kisutu katika hatua ya upelelezi na baadaye itahamishiwa Mahakama Kuu kusikilizwa.
Wanavyosajiliwa Septemba, Shirika la Habari la Uingereza (BBC), lilitoa taarifa fupi ya namna vijana walivyokuwa wakisajiliwa kujiunga na kundi la kigaidi la Al Shabaab katika pwani ya Kenya.
Taarifa hiyo ilitoka baada ya Al Shabaab kukiri kufanya shambulizi la kigaidi katika jengo lenye maduka makubwa la Westgate jijini Nairobi, ambako zaidi ya watu 60 waliuawa na mamia kujeruhiwa.
 
Uchunguzi wa BBC, ulibaini kuwa vijana hao kabla ya kusajiliwa walikuwa wakipitia mafunzo yanayopotosha itikadi za dini katika kuwaandaa kujiunga na kundi la Al Shabaab.
 
Vikao vya kusajili vijana hao ilidaiwa huanza na viongozi wa dini walio tayari kutoa mafunzo hayo, ili watoe hotuba za namna hiyo kwa vijana.
 
Uchunguzi huo umebaini kuwa vijana hao, hufundishwa kujitolea kupigania kile wanachosema ni dini, na baadaye hupelekwa vijijini katika maeneo yanayopakana na fukwe za bahari kujiandaa na safari kwenda Somalia.
-Habari leo
TOA MAONI YAKO KUHUSU HABARI HII
KAMA UMEGUSWA NA HABARI ZETU, TUNAOMBA UUNGANE NASI KATIKA PAGE YETU YA FACEBOOK HAPO CHINI. BOFYA "LIKE" KAMA BADO HUJA LIKE PAGE YETU.
 

KILELE CHA HABARI Copyright © 2014 -- Template created by Mbatta -- Powered by Kilelechahabari