Like Us On Facebook

BRANDS AGOMA KUSAINI MKATABA MPYA YANGA

                                                                        Ernie Brandts.
KOCHA Mkuu wa Yanga, Ernie Brandts, yupo katika majadiliano ya kuongeza mkataba mpya na klabu hiyo, lakini imefahamika kuwa, raia huyo wa Uholanzi, amegomea jambo moja katika mkataba huo mpya.
Taarifa kutoka kwa chanzo chetu cha habari imesema uongozi wa Yanga kupitia kwa mwenyekiti Yusuf Manji, ulizungumza na kocha huyo kwa lengo la kutaka kumsainisha mkataba wa miaka miwili, lakini Brandts aligomea ombi hilo na kutaka mwaka mmoja pekee.
Taarifa hiyo imesema sababu kubwa ya Brandts kugomea kusaini mkataba wa muda mrefu ni kutokana na kipengele kimoja kilichopo katika mkataba huo, kinachomtaka kulipa kiasi cha fedha endapo ataamua kuachana na timu hiyo.
“Brandts alikataa mbele ya mwenyekiti (Manji), ambaye alimtaka kuongeza mkataba wa miaka miwili kutoka ule mmoja wa awali ambao sasa unafikia mwisho, akasema kama ataongeza mkataba anataka uwe wa mwaka mmoja pekee.
“Kikubwa kilichomfanya Brandts kukataa ombi hilo la mwenyekiti ni kutokana na kipengele kilichopo katika mkataba huo ambacho kinamtaka kulipa mshahara wake wa mwezi kama akiamua kuachana na timu hiyo, jambo ambalo yeye anaona kama atakubali mkataba mrefu linaweza kumsumbua.”
Mkataba wa sasa wa Brandts ambao aliusaini mwezi Septemba, mwaka jana, wakati anatua katika timu hiyo, unafikia tamati mwezi huu, ingawa tayari ameshaanza mazungumzo juu ya kuongeza muda zaidi kusalia katika kikosi hicho, alichokipa taji la ubingwa wa Bara msimu uliopita.
TOA MAONI YAKO KUHUSU HABARI HII
KAMA UMEGUSWA NA HABARI ZETU, TUNAOMBA UUNGANE NASI KATIKA PAGE YETU YA FACEBOOK HAPO CHINI. BOFYA "LIKE" KAMA BADO HUJA LIKE PAGE YETU.
 

KILELE CHA HABARI Copyright © 2014 -- Template created by Mbatta -- Powered by Kilelechahabari