HATUA ya Rais Jakaya Kikwete kuridhia kutengua uteuzi wa mawaziri wanne, sasa ina kila dalili za kumpa nafasi ya kuchukua uamuzi wenye mwelekeo mpya ndani ya muda mfupi ujao kuanzia sasa...
Ni
katika mwelekeo huo, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, ambaye naye alitakiwa
na wabunge kujiuzulu, licha ya juzi kutokuwa tayari kulizungumzia jambo
hilo wakati akitangaza uamuzi wa Rais kutengua uteuzi wa mawaziri hao
wanne, anaaminika kutangaza uamuzi huo huku hatma yake ya kuondoka
madarakani ikiwa imezungukwa na wingu la shaka.
Ingawa hadi sasa
Pinda mwenyewe amekwishasema yuko tayari kung’oka na kwamba atafurahi
kama uamuzi huo utachukuliwa dhidi yake, lakini hatua iliyochukuliwa na
Rais Jakaya Kikwete sasa inadhihirisha kuwepo kwa dalili za kutaka
kumnusuru kiongozi huyo dhidi ya shinikizo la wabunge, ambao mara kwa
mara wamekuwa wakimtaka ang’oke, wakimtuhumu kwa uzembe.
Baadhi ya wadadisi na wafuatiliaji wa mambo waliochambua uamuzi huu
wa sasa wa Rais Kikwete, wanaeleza kuwa huenda kiongozi huyo akawa
anatumia staili ile ile aliyoitumia mwaka mmoja uliopita kumnusuru
Pinda.
Wanaeleza kuwa, mwaka 2012, Kikwete alilazimika kufanya
mabadiliko ya Baraza la Mawaziri kwa kuwaweka kando mawaziri nane ambao
wabunge walikuwa wakishinikiza wang’olewe pamoja na Pinda, baada ya
kukasirishwa na ripoti ya Mkaguzi Mkuu na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali
(CAG), iliyowatuhumu mawaziri hao kwa ubadhirifu.
Hata hivyo,
baada ya kufanya mabadiliko hayo, yaliyoshuhudia mawaziri wa Nishati na
Madini, William Ngeleja, Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige, Afya Hadji
Mponda, Viwanda na Biashara Cyril Chami, Uchukuzi, Omari Nundu na
wengine, Rais Kikwete hakumuondoa Pinda na tishio la wabunge kutaka
kumuondoa kwa kura ya kutokuwa na imani naye nalo lilififishwa na hatua
hiyo.
Wakati wadadisi na wachambuzi wa mambo wakiwa na mtizamo
huo, zipo taarifa zinazoeleza kuwa ugumu wa Rais Kikwete kuchukua hatua
ya kumuondoa Pinda unatokana na hatua yake ya kutaka kuinusuru serikali
na mzigo wa gharama za kuwalea mawaziri wakuu pindi wanapoondoka kwenye
nyadhifa zao.
Hatari hiyo ya serikali kubaki na mzigo mkubwa wa
viongozi wakuu wastaafu, ndiyo inayotajwa wakati fulani mwaka 1994
kumlazimisha Rais Ali Hassan Mwinyi kumrudisha kwenye nafasi ya uwaziri
mkuu, Cleopa Msuya, aliyepata kuhudumu kwenye nafasi kama hiyo wakati wa
utawala wa Mwalimu Julius Nyerere.
Hadi sasa Tanzania ina
mawaziri wakuu wastaafu watano, ambao ni John Malecela, Cleopa Msuya,
Jaji Joseph Warioba, Frederick Sumaye na Edward Lowassa.
Hata
hivyo, taarifa ambazo RAI Jumapili limezipata zinaeleza kuwa, Pinda
binafsi yuko tayari kukabidhi madaraka, ingawa uamuzi huo haijulikani
utachukuliwa namna gani na Rais Kikwete pindi atakaporejea Alhamisi wiki
hii, akitokea Marekani, alikokuwa kwenye matibabu.
Kwa mujibu wa
taarifa hizo zilizolifikia gazeti hili, tayari Pinda amemueleza Rais
Kikwete juu ya azma yake hiyo, huku nyingine zikieleza kuwa
amekwishamuandikia barua ya kujiuzulu.
Ingawa si Pinda wala Ikulu
waliopatikana kuthibitisha taarifa hizo hadi tunakwenda mitamboni usiku
wa kuamkia leo, ni wazi kwamba, hatua ya sasa ya Rais Kikwete inakuja
kama mbinu ya serikali yake kutaka kujisafisha kupitia mabadiliko hayo
ya Baraza la Mawaziri, ili kukwepa lawama ambazo zimekuwa zikielekezwa
mara kwa mara na jamii dhidi ya serikali yake kuhusu vitendo mbalimbali
vya ubadhirifu na ukiukwaji wa haki za binadamu.
Tayari mawaziri wawili majina yao yameanza kutajwa kurithi nafasi ya Pinda, ikiwa ataondoka katika nafasi hiyo.
Mawaziri hao ni Waziri wa Miundombinu, Dk. John Magufuli na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Uhusiano na Uratibu, Stephen Wassira.
Aidha
kitendo hicho cha Rais kuamua kutengua uteuzi wa mawaziri wa aina ya
Emanuel Nchimbi wa Mambo ya Ndani, Balozi Khamis Kagasheki wa Maliasili
na Utalii, na David Mathayo wa Kilimo kwa tuhuma zilizotokana na
Operesheni Tokomeza, inatajwa kuliweka njia panda Baraza zima la
Mawaziri, hususan wale wanaotajwa kuwa ni mawaziri mizigo.
Taarifa
zilizolifikia gazeti hili zinaeleza kuwa uamuzi huo wa Rais Kikwete
umewashtua mawaziri karibu wote, huku baadhi yao wakipata shaka kama
wataendelea kubaki katika nyadhifa zao.
Ni hatua hiyo pia
inatajwa kumpatia nafasi ya kuwaondoa au kuwahamisha wizara mawaziri
wengine, wakiwamo wale waliopachikwa jina la mawaziri mizigo pindi
atakapofanya mabadiliko ya Baraza la Mawaziri.
Mawaziri
wanaotajwa kuwa ni mizigo na ambao tayari wamekwishahojiwa na Kamati Kuu
ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ni pamoja na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya
Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu
(Tamisemi), Hawa Ghasia.
Wengine ni Waziri wa Kilimo, Chakula na
Ushirika, Christopher Chiza, Waziri wa Fedha, William Mgimwa, Waziri wa
Viwanda na Biashara, Dk Abdallah Kigoda, na Waziri wa Nchi Menejimenti
na Utumishi wa Umma, Celine Kombani.
Katika mabadiliko hayo ya
Baraza la Mawaziri yanayotarajiwa kufanywa ndani ya muda mfupi, pia
huenda yakatoa nafasi kwa baadhi ya mawaziri ama kuondoka au kubaki,
lakini pia kuwajumuisha wapya.
Miongoni mwa wanaotajwa
kujumuishwa katika baraza jipya la Mawaziri ni pamoja na Dk. Asha Rose
Migiro, ambaye hivi karibuni Rais Jakaya Kikwete alimteua kwenye nafasi
ya ubunge.
-RAI JUMAPILI