Like Us On Facebook

WAASI WA M23 WAKUBALI KUWEKA SILAHA CHINI KWA MASHARTI KADHAA



Wakati vikosi vya Umoja wa Mataifa vikisitisha kwa muda operesheni ya kukabiliana na Kundi la M23 Mashariki kwa Jamhuri ya Demokrasia ya Congo, ili kupisha mazungumzo ya amani, kundi hilo limesema liko tayari kuweka silaha chini. 

Mazungumzo ya kutafuta suluhu ya mapigano kati ya kundi hilo na Jeshi la DRC, yalitarajiwa kuanza jana mjini Kampala,Uganda.
 

Msemaji wa kundi hilo , Bertrand Bisimwa, alisema waasi hao wako tayari kuweka chini silaha lakini mpaka Serikali ya Congo itapotekeleza masharti kadhaa.
 

Kwa mujibu msemaji huyo, masharti hayo ni pamoja kutafutiwa ufumbuzi kwa kadhia inayowahusu wanamgambo wa Kihutu wenye asili ya Rwanda walioko DRC.

Waasi pia wanataka kurejea nchini Congo kwa wakimbizi wanaoishi katika kambi mbalimbali katika nchi jirani za Rwanda, Uganda na Burundi.


Msemaji huyo amesema kama masharti hayo yatatekelezwa basi waasi hao wako tayari kusitisha mapigano na kurejea katika maisha ya kawaida.
 

Kauli hiyo imekuja wakati vikosi vya kimataifa vinavyoundwa na askari kutoka nchi za Tanzania, Afrika Kusin na Malawi, vikifanikiwa kuwafurusha wanamgambo hao kutoka katika maeneo waliyokuwa wameteka.


Katika hatua nyingine, ujumbe wa kwanza wa kundi la waasi wa M23 uliwasili katika mji wa Kampala kwa ajili ya kushiriki mazungumzo ya amani ambayo pia yatahusisha maofisa wa serikali ya Congo.

Katika taarifa yao, waasi hao walisema kuwa walikuwa wakiwasubiri wajumbe wa Serikali ili kuanza tena mazungumzo ya amani hayo.
 

Kuanza kwa mazungumzo hayo kunafuatia juhudi zilizofanywa na viongozi wa nchi za Maziwa Makuu ambao waliweka muda wa siku tatu kuanza upya kwa mazungumzo baina ya waasi wa M23 na serikali ya Congo yenye lengo la kufikia makubaliano ya kumaliza mapigano.

-Mwananchi
TOA MAONI YAKO KUHUSU HABARI HII
KAMA UMEGUSWA NA HABARI ZETU, TUNAOMBA UUNGANE NASI KATIKA PAGE YETU YA FACEBOOK HAPO CHINI. BOFYA "LIKE" KAMA BADO HUJA LIKE PAGE YETU.
 

KILELE CHA HABARI Copyright © 2014 -- Template created by Mbatta -- Powered by Kilelechahabari