
Wakati vikosi vya Umoja wa Mataifa vikisitisha kwa muda operesheni ya kukabiliana na Kundi la M23 Mashariki kwa Jamhuri ya Demokrasia ya Congo, ili kupisha mazungumzo ya amani, kundi hilo limesema liko tayari kuweka silaha chini.
Mazungumzo ya kutafuta suluhu ya mapigano kati ya kundi hilo na Jeshi la DRC, yalitarajiwa kuanza jana mjini Kampala,Uganda.
  
                               Msemaji wa kundi hilo , Bertrand Bisimwa, alisema  waasi hao wako tayari kuweka chini silaha lakini mpaka Serikali ya Congo  itapotekeleza masharti kadhaa.
  
                               Kwa mujibu msemaji huyo, masharti hayo ni pamoja  kutafutiwa ufumbuzi kwa kadhia inayowahusu wanamgambo wa Kihutu wenye  asili ya Rwanda walioko DRC.
                               Waasi pia wanataka kurejea nchini Congo kwa  wakimbizi wanaoishi katika kambi mbalimbali katika nchi jirani za  Rwanda, Uganda na Burundi.
                               Msemaji huyo amesema kama masharti hayo  yatatekelezwa basi waasi hao wako tayari kusitisha mapigano na kurejea  katika maisha ya kawaida.
  
                               Kauli hiyo imekuja wakati vikosi vya kimataifa  vinavyoundwa na askari kutoka nchi za Tanzania, Afrika Kusin na Malawi,  vikifanikiwa kuwafurusha wanamgambo hao kutoka katika maeneo waliyokuwa  wameteka.
                               Katika hatua nyingine, ujumbe wa kwanza wa kundi  la waasi wa M23 uliwasili katika mji wa Kampala kwa ajili ya kushiriki  mazungumzo ya amani ambayo pia yatahusisha maofisa wa serikali ya Congo.
                               Katika taarifa yao, waasi hao walisema kuwa walikuwa wakiwasubiri wajumbe wa Serikali ili kuanza tena mazungumzo ya amani hayo.
  
                               Kuanza kwa mazungumzo hayo kunafuatia juhudi  zilizofanywa na viongozi wa nchi za Maziwa Makuu ambao waliweka muda wa  siku tatu kuanza upya kwa mazungumzo baina ya waasi wa M23 na serikali  ya Congo yenye lengo la kufikia makubaliano ya kumaliza mapigano.
-Mwananchi
-Mwananchi

